Friday 30 September 2016

NI SIMBA NA YANGA LEO TAIFA


simba_v_yanga_bannerV 1
Ligi kuu Vodacom itaendelea leo ambapo kutakuwa na mchezo mmoja tu utakaowakutanisha watani wa jadi, Young Africans na Simba katika dimba la Taifa, Dar es Salaam.
Siku ya Jumapili, michezo itakuwa mitano ambapo Mbeya City itaikaribisha Mwadui kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya. Majimaji itakuwa mwenyeji wa Stand United kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea wakati African Lyon itakuwa mgeni wa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Manungu, Mvomero mkoani Morogoro
. Kwa upande wa Mbao baada ya kucheza na Ruvu Shooting wiki iliyopita, ilibakia Mlandizi mkoani Pwani kusubiri kucheza na JKT Ruvu Jumapili kwenye Uwanja wa Mabatini huko Mlandizi wakati Kagera itaikaribisha Tanzania Prisons kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba mkoani Kagera.

Baraza La Wawakilishi Labariki SMZ ‘Kumpotezea’ Maalim Seif.

Tarehe October 1, 2016
maalim-seif-new-oneV 1

Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wameunga mkono marekebisho ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kwa ajili ya kumpa uwezo Rais kuteua wajumbe wa Baraza bila ya kushauriana na kiongozi wa upinzani huku wakitaka marekebisho mengine zaidi kwa lengo la kuleta ufanisi.

Mwakilishi wa Jimbo la Shauri Moyo, Hamza Hassan Juma alisema wakati umefika sasa kwa Katiba ya Zanzibar izingatie demokrasia ya mfumo wa vyama vingi kwa vitendo na kuacha kuweka kipaumbele kwa vyama vya CCM na CUF.

Alisema athari za kuvishirikisha vyama hivyo, ikiwemo katika Katiba imeanza kuonekana ambapo mwaka jana viongozi wa CUF walisusia Baraza la Wawakilishi wakati wa kupitisha bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Naye Mwakilishi wa Jimbo la Chaani, Nasir Abdulatif Jussa (CCM) alisema marekebisho yatakayopitishwa na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi yatampa uwezo mkubwa Rais wa Zanzibar sasa kuchagua wajumbe wa Baraza la Wawakilishi bila ya kupata ushauri kutoka kwa mtu yeyote.

Akitoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Said Hassan Mzee alisema marekebisho hayo ni muhimu ambayo yataondoa masharti na kumpa uwezo Rais kushauriana na kiongozi wa upinzani ambaye kwa sasa hayupo.

Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi walipitisha muswada huo wa Marekebisho ya 11 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 ambayo sasa yatampa nafasi Rais wa Zanzibar kuchagua wajumbe wawili wa Baraza la Wawakilishi katika nafasi 10 bila ya kushauriana na kiongozi wa upinzani ambaye katika muundo wa Baraza la Wawakilishi la sasa hayupo.

Majaliwa Atimiza Ahadi, Ahamia Rasmi Dodoma

Tarehe October 1, 2016
downloadV 1

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amehamia rasmi Mkoani Dodoma jana Ijumaa Septemba 30, 2016.

Majaliwa aliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Dodoma majira ya saa 10:07 jioni akiwa ameongozana na Mkewe na kupokelewa na viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Kazi na Walemavu, Jennister Mhagama.

Baada ya kuwasili Uwanjani hapo, Majaliwa alikwenda moja kwa moja kwenye makazi yake mapya yaliyopo eneo la Mlimwa na kupokelewa na wazee wa Mkoa wa Dodoma na viongozi wa dini.

Wakazi wa Dodoma walionekana kumshangilia Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa pembezoni mwa barabara inayoelekea katika makazi yake huku wakimpungia kwa majani kama ishara ya amani huku langoni mwa nyumbani kwake kukiwa kumejaa bajaji na pikipiki.

Majaliwa ametimiza ahadi yake ya kuwa wa kwanza kuhamia Mkoani Dodoma licha ya kuahirisha hapo mwanzo katika tarehe ya awali aliyoahidi kuhamia ya Septemba Mosi, mwaka huu.

Kauli Ya Serikali,Tangazo La Ajira Mpya 1000

Tarehe October 1, 2016
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika utumishi wa Umma, Bi. Riziki Abraham.V 1
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika utumishi wa Umma, Bi. Riziki Abraham.

Hatimaye,serikali imetoa kauli yake kufuatia kusambaa katika mitandao ya kijamii Tangazo lenye kichwa cha habari ‘’Sekretarieti ya Ajira yatangaza zaidi ya nafasi za kazi 1,000.

Kwa mujibu wa Katibu wa Sekretarieti ya Ajira amesema kuwa taarifa hiyo haina ukweli wowote na inalenga kuupotosha Umma, hivyo wananchi wote wanapaswa kuipuuza.

Tangazo hilo limeonyesha kuwa Serikali kupitia Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma inawatangazia watanzania wenye sifa na uwezo kujaza jumla ya nafasi wazi za kazi 1,101 kwa niaba ya waajiri mbalimbali Serikalini.

Ameongeza kuwa Matangazo yote ambayo hutolewa na Serikali kupitia Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma ni lazima yaonekane kwenye Tovuti ya Sekretarieti ya Ajira www.ajira.go.tz au portal ya Ajira ambayo niportal.ajira.go.tz.

“Kama mnavyofahamu hivi karibuni Serikali ilitoa taarifa ya kusitisha Ajira mpya Serikalini kwa ajili ya zoezi la uhakiki wa Watumishi hewa kama ambavyo taarifa ilivyotolewa hapo awali, kwa kuwa zoezi hilo bado halijakamilika tunaomba wananchi wote na wadau wa Sekretarieti ya Ajira waendelee kuvuta subira hadi pale zoezi hilo litakapokamilika na taarifa rasmi itatolewa na Mamlaka husika.”Alisisitiza Katibu.

Sekretarieti ya Ajira inapenda kuomba radhi kwa wale wote waliopata usumbufu kutokana na tangazo hilo lenye nia ya kupotosha Umma.

Thursday 29 September 2016

JPM Atamani Mitandao Ya Kijamii Izimwe

Tarehe September 29, 2016
mitandao-ya-kijamiiV 1

Rais Magufuli, Dtk. John Pombe Magufuli amesema anatamani malaika ashuke azime mitandao ya kijamii na kurudi baada ya mwaka 1 ili ikute hatua kubwa za kimaendeleo tulizopiga.

Ameyasema hayo wakati wa uzinduzi wa ndege mbili aina ya Bombadier Q400, ambazo zimewasili nchini rasmi kutoka nchini Canada. Amesema katika mitandao ya kijamii watu wengi wanaandika mambo bila kuwa na taarifa sahihi.

“No research no right to speak,” amesema Rais Magufuli akielezea sababu zake za kutaka mitandao ya kijamii ipotee kwa mwaka mmoja.

Uingereza Yadondosha Bilioni 6 Maafa Tetemeko Kagera

Tarehe September 29, 2016
1-2V 1
Uingereza imetoa mchango wa Shilingi Bilioni 6 kwa Serikali ya Tanzania kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa miundombinu ya shule zilizopata madhara kufuatia tetemeko la ardhi lililotokea katika Mkoa wa Kagera tarehe 10 Septemba, 2016.
Mchango wa fedha hizo umewasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Balozi wa Uingereza hapa nchini Mhe. Sarah Catherine Cooke, Ikulu Jijini Dar es Salaam muda mfupi baada ya Balozi huyo kuwasilisha hati zake za utambulisho.
Balozi Sarah Catherine Cooke amemueleza Rais Magufuli kuwa pamoja na kutoa mchango wa fedha hizo Waziri Mkuu wa Uingereza Mhe. Theresa May anatoa pole kwa Serikali ya Tanzania na kwa familia zote zilizopatwa na madhara ya tetemeko hilo na kwamba Uingereza imeona ishirikiane na Tanzania katika kukabiliana na madhara hayo.
“Uingereza imeguswa sana na maafa yaliyowakumba wananchi kufuatia tetemeko lililotokea Kagera, tunapenda kuona wananchi wanasaidiwa na wanafunzi wanaendelea na masomo” amesema Balozi Sarah Catherine Cooke.
Kwa Upande wake Rais Magufuli amemshukuru Waziri Mkuu wa Uingereza kwa mchango huo ambao utasaidia juhudi za Serikali za kuhakikisha inarejesha miundombinu iliyoharibika zikiwemo shule.
“Mhe. Balozi Sarah Catherine Cooke naomba unifikishie shukrani zangu za dhati kwa Waziri Mkuu wa Uingereza Mhe. Theresa May na umueleze kuwa kwa niaba ya watanzania hususani waliopatwa na madhara ya tetemeko la ardhi tumeguswa sana na moyo wake wa upendo kwetu,” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli na Balozi Sarah Catherine Cooke pia wamezungumzia uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Uingereza ambapo Rais Magufuli ametoa wito kwa Balozi huyo kuendelea kuwahamasisha wafanyabiashara na wawekezaji wa Uingereza kuongeza uwekezaji wao hapa nchini na kwamba Tanzania itaendeleza na kukuza uhusiano huo.
“Uingereza ni rafiki na ndugu wa kweli na wa kihistoria kwa Tanzania, tunatambua kuwa nchi yenu ni mdau mkubwa na muhimu wa maendeleo yetu, hivyo tusingependa kupoteza rafiki na ndugu yetu, tuendelee kushirikiana kwa manufaa ya wananchi. 
“Natambua kuwa Uingereza ina utaalamu mkubwa katika masuala ya gesi hivyo nawakaribisha waje wawekeze katika sekta ya gesi,” amesisitiza Rais Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli amesema Serikali itahakikisha fedha zote zinazotolewa kwa ajili ya kusaidia kukabiliana na madhara ya maafa ya tetemeko la ardhi lililotokea mkoani Kagera zinafikishwa kwa walengwa na ameonya kuwa watakaothubutu kuiba fedha hizo watashughulikiwa.
Dkt. Magufuli amebainisha kuwa baada ya kutengua uteuzi na kuchukua hatua nyingine dhidi ya aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera Bw. Amantius Msole na Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba Bw. Steven Makonda pamoja na kumsimamisha kazi Mhasibu Mkuu wa Mkoa wa Kagera Bw. Simbaufoo Swai, amemtaka Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Dkt. Charles Kimei awachukulie hatua watumishi wa Benki hiyo walioshirikiana na watumishi hao kufanya njama za kuanzisha akaunti nyingine ya benki yenye jina linalofanana na akaunti rasmi ya “Kamati ya Maafa Kagera” kwa lengo la kujipatia fedha”
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
28 Septemba, 2016

Wednesday 28 September 2016

JPM Amwaga Cheche Akizindua Ndege 2 Mpya

Tarehe September 28, 2016
1V 1
Ndege mpya za Serikali zinatarajiwa kufika katika viwanja 12 nchini ikiwemo Dar es Salaam, Zanzibar, Mwanza, Arusha, Bukoba, Tabora na Mbeya, imefahamika.
Hayo yamesemwa leo na Rais, Dkt. John Pombe Magufuli leo katika Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam katika uzinduzi wa ndege mbili mpya za Serikali aina ya Bombardier Q400.
Amewataka Watanzania kutopuuza vitu vyao na kudai kuwa wengine wamezisema vibaya na kuzilinganisha mwendo wake na bajaji.
“Wapo waliosema ndege hizi hazitembei ni kama bajaji, hebu fikiria zimetokea Canada mpaka Dar es Salaam, zimekujaje?,” amehoji Rais Magufuli na kuwataka wale wote wasiozitaka wakae kimya kuliko kuongea uongo.
Amesema kuwa mazungumzo yanaendelea ili kuhakikisha zinapatikana ndege zingine mbili kubwa zenye uwezo wa kubeba abiria 160 hadi 240 zitakazokuwa na uwezo wa kusafiri kutoka Dar es Salaam hadi Marekani na China bila kutua mahali popote.
Ameitaka bodi mpya ya ATCL kutoogopa kupunguza wafanyakazi katika shirika hilo na kuwachambua kama karanga kama Saida Karoli anayosema na kudai kuwa kama waliweza kuunguza wafanyakazi zaidi ya 500 kutoka NIDA ndio sembuse wafanyakazi wa ATCL.
“Ndani ya ATCL kuna wake wa mawaziri wameng’ang’ania tu wakati hata shirika lenyewe halizalishi. Kama mfanyakazi unataka kuendelea kufanya kazi ATCL, ni lazima utubu, na uwe tayari kuwatumikia watanzania,” amesema.
Amesema wafanyakazi wa ATCL wasiokuwa waaminifu walikuwa wakinunua mafuta hewa na kudai kuwa ndege imeenda Mwanza kumbe ipo Uwanja wa Ndege Dar huku wengine wakijilipa posho za shilingi 50,000 kila mara wanapotembelea Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam.
“Tumeamua kununua ndege na kuzikodisha kwa ATCL na sasa muda wa kucheza umekwisha kwani ilikuwa haijiendeshi kibiashara. Walikuwa wapo wapo tu, wanategemea serikali kila kitu,” ameongeza.
Aidha, amelitaka shirika hilo kutokubali kusafirisha viongozi wa serikali bure bila ya kujali ni nani. Awe Waziri Mkuu, aawe Waziri Mbawara au hata mimi Rais ni lazima wote tulipe gharama ya nauli stahiki na hivyo ndivyo biashara inavyotakiwa kuwa huku akiwataka kuachana na mfumo wa kukatisha tiketi kutumia mawakala.

Beki Wa PSG Ahakumiwa Kwenda Jela

Tarehe September 28, 2016
serge-aurier-548645265

Beki wa Paris StGermain, Serge Aurier ambaye ni raia wa Ivory Coast amehukumiwa kwenda jela miezi miwili kutokana na kukutwa na kosa la kumfanyia fujo askari polisi nchini Ufarasa.

Beki huyo machachari wenye umri wa miaka 23 alifanya kosa hilo jijini Paris, Mei 30, mwaka huu ambapo alimshambulia na kumtolea maneno makali Ofisa wa polisi.

Mbali na adhabu hiyo pia amepigwa faini ya euro 600 na mahakama na zinaweza kuongezeka euro 1,500.

Mchezaji huyo anatarajiwa kuwemo katika kikosi cha PSG kitakachocheza keshokutwa Jumatano katika Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Ludogorets, mpaka sasa ameshaichezea PSG mechi 5 msimu huu na kutoa asisti kwa Edinson Cavani katika mechi dhidi ya Arsenal, wiki mbili zilizopita.

Naye mwanasheria wa mchezaji huyo amesema, atakata rufaa kupinga adhabu hiyo, lakini bado kanuni zinamruhusu kuibadili na kuifanya kuwa adhabu ya kuitumikia jamii badala ya kwenda jela.

Watatu Mbaroni Kwa Kuozesha Wanafunzi

kamanda-george-kyando

Wazazi watatu washikiliwa na polisi mkoani Rukwa, akiwemo mume na mke, kwa kosa la kuozesha watoto wao wa kike wenye umri wa miaka 15 waliokuwa wakisoma darasa la sita katika Shule ya Msingi Chipu katika Kata ya Kasense kwenye Manispaa ya Sumbawanga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, George Kyando, alithibitisha kukamatwa kwa wazazi hao na msichana mmoja, huku Polisi ikiendelea kumsaka msichana mwingine na mumewe.

Wazazi waliokamatwa wametajwa kuwa ni Sabastian Sangu na mkewe Hilda Mizengo na mzazi mwingine wa kiume ni Misri Mwanakatwe.

Inadaiwa kuwa mmoja wa watoto hao aliyeozeshwa kijijini humo anashikiliwa na Polisi kwa mahojiano huku mwanamume wake anayedaiwa kuwa ni mtoto wa mwalimu mstaafu, aitwae Daud Kwitwa, kutoroka.

Msichana mwingine na mwanamume aliyeozeshwa walitoroka kijijini humo na kwenda katika kitongoji cha Malangali, Manispaa ya Sumbawanga mkoani humo ambapo wanadaiwa kufunga ndoa Agosti mwaka huu katika Kanisa Katoliki la RohoMtakatifu, Jimbo la Sumbawanga, lililopo kwenye kitongoji cha Malangali.

Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, Dk Halfani Haule amesema, walikamatwa Septemba 29,, wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika Shule ya Msingi Chipu akiwa ameongozana na Ofisa Elimu Taaluma wa Manispaa ya Sumbawanga, Frank Sichalwe.

“Nilipata taarifa ya kuwepo kwa watoro sugu shuleni hapo hivyo nilipofika niliingia darasa la sita nikaomba daftari la mahudhurio na kuanza kuwaita wanafunzi jina baada ya jina ndipo ilipobainika kuwa kati ya wanafunzi 142 wanaosoma darasa hilo, 52 ndio waliohudhuria huku 90 wakikosekana shuleni na kudaiwa kuwa watoro sugu,” amesema Haule.

Haule amesema, alipodadisi zaidi wanafunzi wenyewe walianza kueleza kuwa wengi wa watoro wanafanya kazi za vibarua vya kuchunga ng’ombe na kwamba wasichana wawili wameolewa kijijini humo.

Picha Linaendelea, CUF Yamfukuza Uanachama Lipumba

Tarehe September 28, 2016
14516509_315490638818245_7680821203764878117_nV 1

Baraza Kuu la Chama cha Wananchi CUF leo limemtimua uanachama alikyekuwa Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba.

Uamuzi huo umefikiwa leo katika kikao kilichoongozwa na Mbunge wa Tandahimba, Katani Ahmed Katani baada ya kuungwa mkono na wajumbe wote 43 waliohudhuria kikao hicho.

Mashtaka dhidi ya Lipumba alirejea katika nafasi yake ya Uenyekiti kufuatia barua kutoka kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, yaliandaliwa na Sekretarieti ya CUF ikimtuhumu kufanya vurugu, kuharibu mali za chama na kudharau barua ya wito wa chama hicho iliyomtaka kwenda kujitetea.

Mwishoni mwa wiki iliyopita, Lipumba akiongozana na wafuasi wake chini ya ulinzi wa polisi walidaiwa kuvunja geti na milango ya ofisi ya chama hicho katika Makao Makuu Buguruni, Jijini Dar es Salaam na kuingia katika ofisi hizo.

Aidha, Baraza hilo limeukataa ushauri na mwongozo wa Msajili wa Vyama vya siasa alioutoa kwa chama kwa sababu umekiuka matakwa ya Sheria ya Vyama Vya Siasa ya Tanzania, hauna mantiki na mashiko ya kisheria na unakiuka matakwa ya katiba ya CUF.

Baraza hilo pia limesema Kamati ya Uongozi liliyoiunda ndiyo inayotambulika kikatiba hadi hapo atakapochaguliwa Mwenyekiti mpya wa CUF.

Monday 26 September 2016

Jarida La Forbes ‘Lafagilia’ Ndege Mpya Za JPM.

Tarehe September 26, 2016
Moja ya ndege mbili mpya za Serikali aina ya Bombardier Q400.V 1
Moja ya ndege mbili mpya za Serikali aina ya Bombardier Q400.

Jarida mashuhuri duniani la Forbes, limezitaja ndege aina ya Bombardier Dash8 Q400, ambazo tayari Tanzania imezinunua kuwa ni zenye usalama, zinazotumia mafuta kidogo. Limetabiri kuwa zitakuwa nguzo muhimu kwa usafiri wa bei nafuu kwa nchi mbalimbali.

Kwa mujibu wa makala iliyochapishwa na jarida hilo ikiwa na kichwa cha habari “Can Bombardier’s Q400 Save Regional Air Service in the US?”, mwandishi anafafanua faida ya ndege hizo, ikilinganishwa na ndege nyingine zinazofanya usafiri wa ndani nchini Marekani.

“Bombadier ina kasi nzuri na ya kutosheleza mahitaji ya safari za ndani kwa kiwango cha kuwa na faida zaidi kibiashara, ikilinganishwa na ndege nyingine za aina yake kama ATR,” linaandika jarida hilo la Forbes.

Aidha, jarida hilo linataja faida nyingine ya ndege hizo kuwa ni uwezo wa kutumia mafuta kidogo, jambo litakalosaidia kupunguza gharama za usafiri huo wa ndege nchini kwa wasafiri wa ndani. Jarida hilo linafafanua kuwa kiwango kidogo cha mafuta, kinachotumiwa na ndege hizo, kunazifanya kuwa na ufanisi wa asilimia kati ya 48 mpaka 50 zaidi ya ndege nyingine.

Forbes linasisitiza kuwa kutokana na gharama za matengenezo kupanda na gharama nyingine za uendeshaji, ikiwemo mishahara mizuri kwa marubani, kuna uwezekano mkubwa kwa Bombardier kuendeshwa kwa bei rahisi na ikauza tiketi kwa bei rahisi zaidi.

“Kwa sasa tunakadiria kuwa ndege aina ya Bombardier, ndizo zitakuwa mbadala na zitashika njia nyingi za ndani (Marekani) kwa kiasi cha asilimia 50 hadi 60 na zitasaidia kurejesha usafiri uliositishwa kutokana na gharama kubwa kwa ndege nyingine katika viwanja takribani 20,” linafafanua jarida hilo.

Mugabe Atishia Afrika Kujitoa Umoja Wa Mataifa

Tarehe September 26, 2016
Rais Robert Mugabe akihutubia Umoja wa Mataifa (UN).
Rais Robert Mugabe akihutubia Umoja wa Mataifa (UN).

Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe amesema Bara la Afrika lipo tayari kujitoa katika Umoja wa Mataifa (UN) iwapo madai yake ya kutaka mabadiliko katika umoja huo hayatatekelezwa.

Mugabe ametoa kauli hiyo mara tu baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Harare na kupokelewa na mamia ya wanachama wa chama tawala ZANU­PF na kulakiwa akitokea New York, Marekani.

Amesema kuwa Umoja wa Afrika (AU) unajiandaa kuunda kundi la kusimamia kujitoa likijumuisha mataifa mengine kama Urusi, Uchina na India iwapo Baraza la Usalama la UN halitajumuisha wanachama kutoka katika Bara la Afrika hapo mwakani.

Akihutubia Baraza Kuu la UN, Jijini NewYork, Mugabe alizishutumu nchi za magharibi kwa kuchangia kudorora kwa uchumi na kupelekea hali kuwa mbaya sana katika nchi yake.

Sugu ‘Ampoteza’ Mwenyekiti Wa Kampeni.

Tarehe September 26, 2016
Mbunge wa Mbeya mjini Joseph Mbilinyi.V 1
Mbunge wa Mbeya mjini Joseph Mbilinyi.

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Kampeni za Mbunge wa Mbeya Mjini Joseph Mbilinyi Bw.Christopher Mwamsiku amefariki dunia wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Ikonda Wilayani Makete mkoani Njombe.

Mwenyekiti huyo wa Kampeni za Sugu ndiye aliyepigania ushindi wa Kishindo wa Mh.Sugu katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 unaotajwa kuwa uchaguzi wa kihistoria kuwahi kutokea hapa nchini kutokana na ushindani uliokuwepo.

Akizungumzia kumpoteza Mwenyekiti huyo ambaye pia alikuwa katibu wake Sugu alisema hili ni pigo kwake pamoja na Chama kwa ujumla kutokana na mchango mkubwa wa kiongozi huyo. “Nimepata pigo kubwa sana, nimepoteza moja ya nguzo yangu kubwa na chama kwa ujumla.”Alisema Sugu.

Lipumba Aanza Kusaka Mali ZaCUF Zilizotoweka Kiajabu.

Tarehe September25, 2016
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Haruna Lipumba.

V 1Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Haruna Lipumba.

Baadhi ya mali za Chama cha Wananchi (CUF) hazijulikani zilipo na tayari Prof.Ibrahim Lipumba ameanza kuzisaka.

kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa chanzo cha ndani ya CUF zinaeleza kuwa, miongoni mwa mali hizo ni magari matano ya chama hicho.

Taarifa zaidi zinaeleza, kabla ya Prof. Lipumba kuingia Ofisi Kuu ya chama hicho zilizopo Buguruni jijini Dar es Salaam jana mchana, magari hayo yalikuwa tayari yameondolewa.

Na kwamba, juhudi za kutaka kujua magari hayo mahala yalipo zimeanza kuchukuliwa kwa Prof. Lipumba kuwasiliana na baadhi ya viongozi waliokuwa na dhamana na ofisi hiyo kabla ya jana.

“Magari kama sita hayapo ndani ya ofisi hizo, Prof. Lipumba ameanza kuuliza magari hayo yapo wapi?,” kimeeleza chanzo hicho na kuongeza;

Alimpigia Mtatiro (Julius Mtatiro­Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la CUF) lakini alisema hajui, akampigia Paku (Abdalla PakuOfisa Utawala wa CUF) alikata simu na alimpigia Bashange (Joram Bashange Mkurugenzi wa Fedha wa CUF) alimjibu kuwa yupo mkoani.

 Hata hivyo, mtandao huu umemtafuta Abdul Kambaya anayetajwa kuwa mtu wa karibu na Prof. Lipumba ambaye amethibitisha taarifa hizo.

“Ni kweli magari hayapo na Profesa amekuwa akifanya juhudi za kutaka kujua magari hayo yalipo.

“Bado hatujaangalia mambo mengine zaidi lakini kuna baadhi ya vitu havipo na tutaendelea kuangalia mali ipi ya chama na nani anayo,” amesema Kambaya na kuongeza;

“Mali za CUF ni za wanachama wote na hakuna shaka tutajua zilipo. Hatuamini kama zimetoka nje kwa njia za hovyo ila naamini mwenyekiti anataka kujua tu mali hizo zipo wapi kwa kuwa anawajibuka kujua.”

Kambaya amebainishwa kwamba, Prof. Lipumba amekuwa akiwasiliana na baadhi ya viongozi ili kutaka kujua yalipo magari hayo.

“Sijui kwa watu wengine lakini najua kuwa amewasiliana na Bashange ambaye alijibu kwamba yupo nje ya Dar es Salaam,” amesema Kambaya.

Jana kwenye Ofisi Kuu ya chama hicho kulikuwa na hekaheka kutokana na Prof. Lipumba kurejea ofisini hapo akisindikizwa na wafuasi wake. Hatua hiyo iliyokana na taarifa ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini iliyotolewa jana ikieleza kumtambua Prof. Lipumba kwamba ni mwenyekiti halali wa chama hicho kwa mujibu wa taratibu.

“Baada ya upembuzi wangu ni kuwa, Lipumba bado mwenyekiti halali wa CUF na waliofukuzwa, kusimamishwa ni wanachama halali.

“Viongozi ambao uamuzi wao uliathirika na maamuzi ya Baraza Kuu la Uongozi wa Taifa bado ni viongozi halali wa CUF,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo iliyosainiwa Jaji Francis Mutungi, Msajili wa Vyama vya Siasa nchini.

Prof. Lipumba aliandika barua ya kujiuzulu uenyekiti wa chama hicho Agosti mwaka jana kwa madai ya kutoridhishwa na ujio wa Edward Lowassa ambaye baadaye aliteuliwa kuwa mgombea urais wa Chadema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana na kuungwa mkono na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Hata hivyo, Agosti mwaka huu CUF ilimsimamishwa uanachama Prof. Lipumba kwa tuhuma za kuwa kinara wa vurugu zilizosababisha mkutano mkuu maalum wa chama hicho kuvunjika.
Mkutano huo ulifanyika katika Hotel ya Blue Pearl jijini Dar es Salaam, Prof. Lipumba na wafuasi wake waliuvamia na kusababisha kuvunjika.
Wengine ni Magdalena Sakaya, Naibu Katibu Mkuu Bara na Mbunge wa Kaliua; Maftaha Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini na Kambaya.
Uamuzi huo ulitangazwa  rasmi na Nassor Ahmed Mazrui, Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, wakati akitoa taarifa ya Kikao cha Baraza Kuu la Uongozi Taifa (BKUT), kilichofanyika mjini Zanzibar mwezi uliopita.

Saturday 24 September 2016

Majaliwa Atafuna Mfupa Ulioshindikana Kwa Siku 10

Tarehe September 24, 2016
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.V 1
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa amefanikiwa kumaliza mgogoro uliodumu kwa muda mrefu kati ya Taasisi ya Hifadhi ya Bahari na Maeneo Tengefu na Halmashauri ya Mafia.
Baada kupewa taarifa ya Mgogoro huo Majaliwa ametoa muda wa siku 10 kwa Taasisi ya Hifadhi ya Bahari na Maeneo Tengefu kulipa deni la sh. milioni 100 inayodaiwa na Halmashauri ya wilaya ya Mafia.
Deni hilo linadaiwa kutokana na malimbikizo ya miaka mitatu ya maduhuri yatokanayo na makusanyo yanayofanywa na taasisi hiyo katika maeneo ya hifadhi ya bahari wilayani humo.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo Ijumaa jana wakati akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya wilaya hiyo katika ukumbi Caltas akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi siku mbili.
“Waandikieni barua na muitume leo hii kwa njia ya mtandao (email) kuwajulisha kuwa wanatakiwa kulipa deni hilo ndani ya siku 10. Hakikisheni wanalipa deni hili ili Halmashauri iweze kufanya kazi zake vizuri,” amesema.
Waziri Mkuu amesema Serikali inataka kuona Halmashauri hiyo ikinufaika kutokana na vyanzo vyake vya mapato, hivyo haitakuwa tayari kuona ikihangaika.
Waziri Mkuu pia amesema atafuatilia kuona wajibu wa taasisi hiyo na mipaka yao ikiwa ni pamoja na kujua mapato yatokanayo na shughuli hizo katika maeneo ya hifadhi.
Naye mkuu wa wilaya ya Mafia Shaib Nnunduma alisema kuwa miongoni mwa changamoto zinazoikabili wilaya hiyo ni kutolipwa kwa wakati fedha za maduhuri yatokanayo na makusanyo yanayofanywa na Taasisi ya Hifadhi ya Bahari.

Viongozi Wa Dini ‘Wamkingia Kifua’ Rais Magufuli.

Tarehe September 24, 2016
Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhad Mussa Salum.V 1
Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhad Mussa Salum akionyesha gazeti lilitoa taarifa ya uongo.

Viongozi wa Dini nchini, wamesema sio kweli Rais, Dkt. John Pombe Magufuli amekataa kuzungumza wala kuwapuuza kukutana na viongozi hao ambao wamemuomba kukutana naye, tofauti na inavyoenezwa na baadhi ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.

Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhad Mussa Salum, amesema hayo Jijini Dar es Salaam kufuatia taarifa zilizochapishwa na gazeti la Tanzania Daima la Septemba 21 ISSN 0856 9762 toleo na. 4310 na kudai kuwa sio za kweli.

“Taarifa hizo sio za kweli, taarifa hizo zimelenga kumgombanisha Rais na Viongozi wa Dini na watanzania kwa ujumla na hilo halitafanikiwa,” amesema Sheikh Salum.

Aidha Viongozi hao wamesema uamuzi wao wa kumuomba Rais kuonana naye, haujatokana na kuagizwa na UKAWA, bali umetokana na maono waliyopewa na Mwenyezi Mungu.

Amefafanua kuwa Rais Magufuli anawaheshimu sana Viongozi wa Dini na mara zote amekua akiwaomba wamuombee na kusema leo ni siku ya tano tangu wamuandikie barua ya kumuomba kukutana naye na wanaimani Rais atakutana na Viongozi hao.

Ameeleza kuwa Barua hiyo imeandikwa Septemba 19 na kupelekwa siku hiyo hiyo Ikulu, ikiwa imesainiwa na Katibu Mkuu wa Bakwata, Katibu Mkuu wa CCT na Katibu Mkuu wa TEC.

“Naomba watanzania wasisikilize maneno hayo kwasababu hayana nia njema kwa Taifa letu, naamini Mheshimiwa Rais tutaonana nae na tutaongelea mustakbali wa nchi katika mambo mbalimbali,” ameongeza Sheikh Salum.

Akizungumzia utendaji wa Serikali ya Rais Magufuli, Sheikh Salum amesema Rais amerejesha nidhamu Serikalini, ukusanyaji mapato umeimarika na pia pengo kati ya wasionacho na walionacho linaanza kupungua.

Lowassa Aibukia Kagera Kuwafariji Wahanga Wa Tetemeko.

Tarehe September 24, 2016
1-1

Aliyekuwa Mgombea Urais na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, Edward Lowassa amewasili Mjini Bukoba Mkoani Kagera kutembelea na kuwajulia hali wahanga wa tetemeko la ardhi lililotokea Kanda ya Ziwa hasa mkoani humo Septemba 10 na kusababisha vifo vya watu 19 huku wengine zaidi ya 250 wakiachwa na maejeraha mbalimbali.

Lowassa aliyeambatana na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema , Sheikh Katimba, Khamis Mgeja na Mbunge wa Bukoba Mjini, Wilfred Lwakatare waliongozana hadi eneo la Hamugembe na Kashai kujionea madhara ya tetemeko la ardhi.

Akizungumza kwa nyakati tofauti na wananchi wa maeneo hayo, Lowassa aliwapa pole sana kwa yote yaliowafika na kusisitiza kwamba anaamini serikali itachukua jukumu la kuwasaidia.

Aidha, amesema kuwa msaada wake yeye atampatia Mkuu wa Mkoa, Meja Jenerali Mstaafu, Salum Kijuu ili uweze kuwasaidia wananchi wa Kagera.4352whatsapp-image-2016-09-23-at-16-28-26

Friday 23 September 2016

Wazimbabwe Kuwekeza Dodoma.

Tarehe September 23, 2016
downloadV 1
Mbali na uwepo wa wawekezaji wa hapa nchini kuonesha nia ya kuwekeza mkoani Dodoma katika viwanda vya saruji na matairi, wawekezaji kutoka Zimbabwe wanataka kuwekeza katika miundombinu kwa kuweka umeme na maji.
Ofisa Mwandamizi wa Uwekezaji Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu ( CDA), Abeid Msangi amesema, tangu Serikali ya Awamu ya Tano kuanza kufanya utekelezaji wa kuhamia Dodoma, kasi ya uwekezaji na wawekezaji mkoani humo imeongezeka.
Msangi amesema, wawekezaji wa ndani wawili wameomba kupatiwa nafasi ya kuwekeza katika kiwanda cha matairi na mwingine kiwanda cha saruji.
“Kama mambo yataenda vyema katika siku za usoni Dodoma itakuwa na viwanda vya saruji na matairi, mkoa wa Dodoma una rasilimali za kutosha za madini ya kutengeneza saruji ya chokaa huko Itigi na Mpwapwa ambayo ndiyo kiini cha saruji,” amesema Msangi.
Msangi amesema , kwa upande wa wawekezaji hao wanataka kuwekeza na kuweza kuwapatia wananchi wa Dodoma miundombinu bora, maji na umeme.
Msangi amesema,wawekezaji hao ni mapema kuwataja, wanataka kuwekeza katika huduma na hawahitaji ardhi katika hilo zaidi ya eneo la kufanyia kazi na ikikamilika wanaondoka.
Aidha amesema kwamba mamlaka hiyo inaendelea kutafuta mwekezaji kwa ajili ya kurekebisha klabu ya CDA ili iweze kutoa nafasi ya ofisi mbalimbali, Baraza la Taifa la Mazingira (NEMC) nalo limeomba eneo la kujenga ofisi zake.
Katika siku za karibuni Mkurugenzi Mkuu wa CDA, Paskari Muragiri amesema, wamekamilisha zoezi la upimaji wa ardhi kwa ajili ya wizara na ofisi za ardhi na kwamba wanakamilisha data kazi kabla ya kuitoa kwa umma.

Mhadhiri Chuo Kikuu Mbaroni Kwa Kumkashifu Rais Magufuli.

Tarehe September 23, 2016
cs441moxyaqps-mV 1

Jeshi la Polisi Mkoani Iringa limemkamata Mhadhiri wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu cha Mkwawa (MUCE), Dkt. Oscar Magava, 48, kwa kumkashifu Rais, Dkt. John Pombe Magufuli katika mitandao ya kijamii.

Akithibitisha kukamatwa kwa Mhadhiri huyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Julius Mjengi amesema Magava alikamatwa akiwa Sumbawanga na kurudishwa Mkoani Iringa.

Amesema Septemba 15, mwaka huu, Jeshi hilo lilipata taarifa kuwa mhadhiri huyo anatumia mitandao ya kijamii kumkashifu Rais Magufuli na kuamua kumsaka hadi pale walipowasiliana na polisi wa Sumbawanga na kupelekea kukamatwa kwake na kurudishwa Iringa.

Hatahivyo, Kamanda Mgava hakutaja maneno ambayo mhadhiri huyo anadaiwa kuyatumia kumkashifu Rais Magufuli kwa madai kuwa bado wanaendelea na uchunguzi na pale utakapokamilika atafikishwa mahakamani.

Mhadhiri huyo anakuwa mtu wa kumi sasa kukamatwa na Jeshi la Polisi kuusiana na matukio ya kumkashifu Rais Magufuli katika mitandao ya kijamii chini ya Sheria ya Uhalifu wa Mitandaoni.

JPM Ateua Vigogo ATCL.

Tarehe September 23, 2016
Rais, Dkt. John Pombe Magufuli.
Rais, Dkt. John Pombe Magufuli.
1

Thursday 22 September 2016

Makaburi Hewa Tisa Yatengenezwa.

Tarehe September 22, 2016
downloadV 1
Baadhi ya wananchi mkoani Simiyu ambao maeneo yao yanapitiwa na miradi mikubwa ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami wanadaiwa kutengeneza makaburi hewa tisa ili walipwe fidia na tayari wamelipwa sehemu ya fidia hiyo.
Shilingi milioni sita zilitengwa kwa ajili ya kuwalipa fidia wenye makaburi hayo yaliyopitiwa na barabara na wananchi wengi walibainika kujenga makaburi hewa na kudai barabara imeyafuata kwa lengo la kupata fidia hiyo.
Meneja wa Wakala wa Barabara (Tanroads) Mkoa wa Simiyu, Albert Kent amesema, wakati wa kikao cha Bodi ya Barabara mkoani hapa kilichofanyika mjini Bariadi.
Kent amesema, makaburi manne yaligundulika kuwa hewa katika mradi ambao umemalizika ujenzi wake wa Lamadi­Bariadi, ambapo kaburi moja tu lilikuwa halali kati ya matano na katika mradi mpya wa ujenzi wa barabara ya Maswa­Mwigumbi unaojengwa kwa kiwango cha lami, makaburi matano kati ya sita yalikuwa hewa.
“katika makaburi hayo tayari wamiliki walikuwa wamelipwa fidia, ambapo walipata taarifa kutoka kwa raia wema na kuelezwa kuwa baadhi ya makaburi ni hewa, lakini si vizuri watu kuweza kutengeneza makaburi hewa kwa lengo la kujipatia pesa”amesema Kent.
Kent amesema, katika makaburi hayo kiasi cha Sh milioni sita zilitengwa kulipia fidia kwa wananchi ambao makaburi yao yalipitiwa, lakini baada ya kuchunguza Tanroads ililipa Sh 500,000 tu na pesa zilizobaki kurejeshwa serikalini. Aidha, Kent amesema, katika kuhakiki makaburi hayo walikuwa wakiambatana na viongozi wa vijiji, ambapo wamiliki walikuwa wakiamriwa kufukua wao wenyewe kabla ya kulipwa pesa zao.

Mkemia Mkuu Kupima Madereva Walevi.

Tarehe September 22, 2016
mkemiapicha
Serikali imesema inakusudia kuendesha kampeni maalum ya kupima matumizi ya vilevi kwa madereva wanaosafirisha abiria na mizigo ikiwa ni hatua ya kukabiliana na tatizo la ajali za barabarani nchini.
Hayo yamesemwa Jijini Dar es Salaam na Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Samwel Manyele alipokuwa akifungua mafunzo ya siku mbili kwa wadau wa kemikali juu ya matumizi salama ya kemikali nchini. Profesa Manyele alisema utaratibu wa kuwapima madereva hao utaanza hivi karibuni na utawezesha kupunguza tatizo la ajali barabarani na kuvitaka vyombo vya ulinzi na usalama kutoa ushirikiano katika zoezi hilo.
“Madereva wote wanaosafirisha mizigo na abiria watatakiwa kupita kwenye kipimo ambacho kitaonyesha kama madereva hao wanatumia vilevi, hali hiyo itasaidia kutatua tatizo la ajali za barabarani nchini,” amesema Manyele.
Profesa Manyele amesema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kutoa uwezo na uelewa kwa wahusika hasa wasimamizi wa shughuli za kemikali na matumizi salama juu ya kukabiliana na matukio au ajali za kemikali pale yanapotokea.

Madereva Waliotekwa Congo Watoboa Siri Ya Kupona Kwao.

Tarehe September 22, 2016
cs7cadtviaalteeV 1

Madereva wa Tanzania waliokuwa wametekwa na askari wa Kikundi cha Uasi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) wamesema kuwa njaa ya watekaji nduiyo iliowaokoa kirahisi kupitia majeshi ya nchi hiyo.

Mmoja kati ya madereva hao kumi amesema hayo mara tu baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere (JNIA) huku kukiwa na vilio, machozi na furaha kwa ndugu, jamaa na marafiki waliofika kuwalaki na kuwapokea madereva hao.

Dereva huyo, Athumani Fadhili amesema baada ya kuishiwa chakula watekaji hao walilazimika kumtuma mmoja wao ili aende kutafuta chakula maeneo ya Mjini na ndipo alipogundulika na majeshi ya Congo ambayo yaliamua kumfatilia kwa karibu akiwa anarudi ndipo walipoweza kutukomboa.

“Waliorodhesha majina yetu kwa kutumia pasipoti zetu, kutuhoji taarifa kuhusiana na familia zetu, mabosi wetu, kama tumeoa au la na kuziandika. Walitutembeza maeneo ya porini na kila walipokuwa wakihisi majeshi yanawakaribia walikuwa wakituhamisha hadi siku tuliyokombolewa,” amesema Fadhili huku akibubujikwa na machozi.


Lowassa Aitilia Shaka Serikali.

Tarehe September 22, 2016
Edward Lowassa.
V 1Edward Lowassa

 Aliyekuwa Mgombea Urais kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Edward Lowassa, ameelezea wasiwasi wake juu ya dhamira ya Serikali kwa upinzani kutokana na migogoro inayozidi kukua baina ya viongozi wa Mkoa wa Arusha na Chadema na kudai kuwa ni mpango mahususi wa Serikali kutaka kukatisha tama vyama vya upinzani.

Amesema mipango hiyo ya Serikali inalenga kuvikatisha tama vyama vya upinzani ili visitekeleze majukumu yake kwa wananchi.

Lowassa ambaye pia alikuwa Waziri Mkuu kabla ya kuhamia Chadema Julai, mwaka jana, amesema hayo akiwa nyumbani kwake Monduli baada ya kuulizwa kuhusu hali ya kisiasa inayoendelea Mkoani Arusha kati ya viongozi wa Serikali na Chadema ambayo ndiyo inayoongoza Halmashauri ya Jiji la Arusha.

“Kinachoendelea Arusha ni mkakati wa Serikali wa kutaka kukandamiza upinzani na kuvikatisha tamaa vyama vya upinzani ili visitekeleze majukumu yake na mwisho wasifanikiwe katika mambo yao,” amesema Lowassa.

Wednesday 21 September 2016

Kilimanjaro Queens Mabingwa CECAFA, 2016

Tarehe September 21, 2016
Kilimanjaro Queens players celebrate after scoring against Burundi during a warm-up match ahead of the 2016 Cecafa Women Championship at Kaitaba Stadium. PHOTO | FILE
Wachezaji wa Kilimanjaro Queens wakishangilia moja ya magoli yao.

Timu ya Taifa ya Soka ya Wanawake ‘Kilimanjaro Queens’ imeshinda kombe la CECAFA baada ya kuinyuka timu ya Kenya magoli 2­ kwa1 katika fainali iliyopigwa Jijini, Jinja, Uganda.

Magoli ya Queens yaliwekwa kimiani na Wachezaji Mwanahamis Omary (27’) na Stumai Abdallah (44’) huku goli la kufutia machozi la Kenya likifungwa na Nafula (48’).

Hadi kipindi cha kwanza kinaisha Tanzania ilikuwa inaongoza 2­0 na kumiliki sehemu kubwa ya mpira huo na hadi dakika 90 zinamalizika matokeo yakawa 2 kwa­1.

Guardiola Amtaka Toure Aombe Radhi, Vingivevyo ‘Atasugua’ Benchi Daima.

Tarehe September 21, 2016
fulham-v-manchester-city-yaya-toure-hat-trick_3105609
Kocha wa Manchester City, Pep Guardiola amemtaka mchezaji wa klabu hiyo, Yaya Toure kuomba radhi kutokana na maneno mabovu aliyoyasema wakala wake vinginevyo hataichezea timu hiyo.
Toure, 33, ameichezea City mchezo mmoja tu tangu msimu huu uanze na ameachwa rasmi katika kikosi cha City kitakachoshiriki michuano ya Klabu Bingwa Ulaya.
Wakala wake, Dimitri Seluk alikaririwa akisema kuwa kiungo huyo ‘amedhalilishwa’ na Guardiola atapaswa kumuomba radhi kama City haitachukua ubingwa.
Amesema ni lazima Toure aombe msamaha na kama hataki hatacheza kamwe.
Kocha huyo vilevile anataka kuombwa radhi na wakala huyo Seluk na kukiri kuwa ulikuwa uamuzi mgumu sana kumuacha Toure katika kikosi cha ligi ya mabingwa ulaya.
Guardiola ameyasema hayo muda mfupi tu baada ya Toure ambaye pia ni kiungo wa Kimataifa wa Ivory Coast kutangaza kustaafu kuichezea timu ya Taifa ya Ivory Coast
Akiwa ameanza kuichezea timu ya taifa mwaka 2004, Toure ameshinda jumla ya mechi 113 akiwa na timu ya taifa, ikiwa ni pamoja na Kombe la Mataifa ya Afrika, mwaka 2015.
“Baada ya miaka 14 ya kiwango cha juu, nina uhakika kuwa huu ni muda muafaka wa mimi kufanya hivyo,” amesema Toure katika taarifa aliyoitoa huku akikiri kuwa kuandika taarifa hiyo pengine ni moja ya wakati mgumu sana katika maisha yake.

clouds stream