Wednesday 4 June 2014

LAMPARD ATANGAZA KUONDOKA CHELSEA


Lampard anataka kustaaafu ingawa vilabu vingi vinataka kumsajili
Kiungo cha kati wa Chelsea Frank Lampard ametangaza kwamba ataondoka katika klabu hiyo baada ya kuichezea kwa miaka 13.
Mchezaji huyo wa Uingereza mwenye umri wa miaka 35 na ambaye ndiye mfungaji bora zaidi wa mabao katika klabu hiyo kwa jumla ya mabao 211, anamaliza kandarasi yake mwezi huu.
Tangu alipojiunga na klabu hiyo kutoka West Ham mwaka wa 2001, Lampard ameshinda mataji makuu 11, zikiwemo 3 za ligi ya Premier na ile ya vilabu bingwa mwaka wa 2012.
''Klabu hii imekuwa sehemu ya maisha yangu,” alisema Lampard ambaye anaweza kustaafu ingawa vilabu 16 vinataka kumsajili.
Sasa hivi yuko pamoja na kikosi cha Uingereza mjini Miami kabla ya Kombe la Dunia na hatafanya uamuzi wowote kuhusu hatima yake baada ya mashindano hayo.
Baada ya kusajiliwa kwa Euro milioni 11, Lampard aliichezea Chelsea michuano 688 na kumfanya kuwa mchezaji wa tatu kuwahi kuichezea klabu hiyo mechi nyingi zaidi nyuma ya Ron Harris aliyecheza mechi 795 na Peter Bonetti aliyecheza mechi 729.
Katika muda wake kwenye klabu hiyo iliyoko magharibi mwa London, amewahi pia kushinda mataji 4 ya FA, mawili ya ligi na ligi ya Uropa.
''Nilipojiunga na klabu hii nzuri miaka 13 iliyopita, singewahi kuamini kwamba ningekuwa mwenye bahati ya kucheza mechi nyingi na kushiriki ufanisi namna hii,” aliongezea Lampard, mchezaji bora wa mwaka wa Chelsea mara tatu.

clouds stream