Thursday 24 August 2017

Lukuvi Ajibu Lawama Za Sumaye Kunyang’anywa Mashamba

Fredrick Sumaye.
Fredrick Sumaye.
IMG-20170426-WA0006

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe William Lukuvi amesema mtu yoyote asiyelipa kodi ya ardhi na kuendeleza ardhi hiyo, ni sababu tosha ya kunyang’anywa ardhi hiyo pamoja na kufutiwa hati ya umiliki kwa kuwa anaingizia hasara serikali.

Waziri Lukuvi amefunguka hayo ikiwa imepita siku moja tangu kwa aliyekuwa Waziri Mkuu wa Awamu ya Tatu, Mhe. Fredrick Sumaye kudai chanzo cha kupokonywa shamba lake ni siasa tu za yeye kuhama chama cha CCM na kwenda kuupa nguvu upinzani, akielekeza lawama zake kwa Rais Magufuli na Waziri Lukuvi.

“Kila mtu atambue iwe ni kiwanja au shamba kama unatabia ya kutolipa kodi ya ardhi ni sababu tosha ya wewe kunyang’anywa shamba lako au ardhi unayomiliki,” amesema Lukuvi.

Amesema kuna tabia imejitokeza kwa watu wachache kuchukua ardhi kubwa kwa miaka mingi kuliko hata uwiano wa uendelezaji wa ardhi hiyo, kwa mfano kuna hati moja hapa ambayo inapigiwa kelele tokea mwaka 1939 imekuwa ikitembea mikono mwa watu.

“Sasa miaka ile watu walikuwa wachache unapokwenda kuchukua ardhi ya kijiji hekari elfu 60 kwa mfano hivi sasa wananchi utakuwa umewaachia kitu gani?” amehoji Mhe. Lukuvi.

Amesema imekuwa kawaida ya baadhi ya watu wanapowahi maeneo huwa wanakimbilia kuchukua sehemu zenye manufaa makubwa kwa upande wao na mwishowe wanashindwa kuendelezaa maeneo hayo kama walivyoyakimbilia.

“Unawahi kuchukua sehemu zenye manufaa kama mto, ardhi inayolimika, sasa unachukua hekari zote hizo halafu huliendelezi mwishowe shamba hilo hilo tunalikuta Benki umelikopea fedha. Kisha umepata fedha hizo unakwenda kujengea ‘apartment’ sehemu nyingine na kule wananchi wanalimezea mate.Serikali wanatumia nguvu kubwa sana kutuliza wananchi wasivamie hilo shamba, halilimwi, serikali hatupati kodi,” ameongeza Lukuvi.

Kwa upande mwingine, Waziri Lukuvi amesema serikali imekuwa na huruma kwa miaka mingi kwa wananchi wake lakini serikali ya uongozi huu wamekubaliana kila mtu afuate sheria kama inavyotakikana.

clouds stream