Wednesday 18 October 2017

Uchaguzi 2017: Kamishna wa tume ya uchaguzi Kenya Roselyn Akombe IEBC ajiuzulu

Roselyn Akombe 6 Julai 201

Roselyn Akombe

Mmoja wa maafisa wakuu wa Tume ya Uchaguzi Kenya (IEBC) Dkt. Roselyn Akombe ametangaza kujiuzulu katika tume hiyo chini ya wiki moja kabla ya uchaguzi mpya wa urais kufanyika nchini humo.
Ametangaza kwamba anahofia usalama wake na hatarajii kurejea Kenya hivi karibuni.
Dkt Akombe ametuma taarifa kutoka mjini New York anakoishi ambapo alikuwa akiufanyia kazi Umoja wa Mataifa kabla ya kujiunga na tume ya IEBC.
Katika taarifa, Dkt Akombe alisema kuwa merejeleo ya uchaguzi utakaofanyika hayaafikii matarajio ya uchaguzi ulio huru na wa haki.
Tume ya IEBC imesema imesikitishwa na hatua ya Dkt Akombe kujiuzulu na kuahidi kutoa taarifa ya kina baadaye. Mwenyekiti Wafula Chebukati anatarajiwa kuhutubia wanahabari baadaye leo.

 "Uamuzi wangu wa kuondoka IEBC utawasikitisha baadhi yenu, lakini si kwa sababu nilikosa kujaribu. Nilijaribu kadiri ya uwezo wangu ukizingatia hali na mazingira yaliyopo. Wakati mwingine, unalazimika kusalimu amri na kuondoka, hasa wakati maisha ya watu yamo hatarini," amesema kwenye taarifa hiyo."Tume sasa imekuwa kama sehemu ya mzozo wa sasa. Tume imo matatani."
"Imekuwa vigumu kuendelea na mikutano ya tume ambapo Makamishna kila wakati wanalazimika kupiga kura kufanya maamuzi kwa kufuata msimamo wao badala ya kuangazia uzito wa jambo linalojadiliwa.

Akombe

"Imekuwa vigumu kutokea kwenye televisheni kutetea misimamo ambayo natofautiana nayo kwa sababu ya kuwajibika kwa pamoja.

"Nimefikia uamuzi kwamba siwezi tena kutoa mchango wa maana kwa Tume na kwa taifa langu kama Kamishna."

Dkt Akombe alitarajiwa kuwa miongoni mwa kundi la maafisa waliokwenda Dubai kuchunguza uchapishaji wa makaratasi ya kupigia kura.

Dkt Akombe alizuru Nyanza na maeneo ya Magharibi, ambayo ni ngome ya upinzani, wiki iliopita huku tume hiyo ikijaribu kuwafunza maafisa watakaosimamia uchaguzi huo.

Roselyn Akombe: Nahofia maisha yangu sirudi Kenya karibuni

Wakuu wa IEBC

Mwenyekiti: Wafula Chebukati

Naibu Mwenyekiti: Consolata Nkatha Maina

Makamishna:

Boya Molu

Paul Kibiwott Kurgat

Abdi Guliye

Margaret Wanjala Mwachanya

Afisa Mkuu Mtendaji/Katibu: Ezra Chiloba

Tume ya Taifa ya Uchaguzi IEBC ilimtangaza Rais Kenyatta kuwa mshindi wa uchaguzi uliofanyika tarehe 8 Agosti, akiwa mbele ya mpinzani wake Raila Odinga wa muungano wa upinzani Nasa kwa zaidi ya kura 1.4 milioni.

Bw Odinga alipinga matokeo hayo mahakamani na Mahakama Kuu ikaamua ulijaa kasoro nyingi na kuagiza uchaguzi mpya ufanyike katika kipindi cha siku sitini.

Tume ya uchaguzi ilitangaza tarehe mpya ya uchaguzi kuwa 26 Oktoba lakini Bw Odinga alijiondoa wiki iliyopita akisema mageuzi ambayo yalifaa kutekelezwa kuhakikisha uchaguzi huru na wa haki hayajatekelezwa.

clouds stream