Tuesday 24 May 2016

Sakata La Bunge ‘LIVE’: Nape Aumbuka Mwanza

Sakata La Bunge ‘LIVE’: Nape Aumbuka Mwanza

Tarehe May 24, 2016NapePHOTO
NapePHOTO
Waziri wa Habari, Nape Nnauye
Kufuatia kuzuia shughuli za Bunge kuonyeshwa moja kwa moja na vituo vya televisheni, Waziri wa Habari, Nape Nnauye juzi alishindwa kuhutubia wapenzi wa muziki jijini Mwanza baada ya wapenzi hao kumpokea kwa kelele za kudai bunge lioneshwe ‘live’.
Juzi, Nape aliyekuwa mgeni rasmi katika tamasha la Jembeka Festival lililofanyika kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, alipokewa na kelele za maneno “Bunge Live” wakati akikaribishwa kuhutubia katika tamasha hilo ambalo lilijumuisha msanii kutoka Marekani, Ne-yo.
“Bunge live, Bunge live, Bunge live,” walipiga kelele mashabiki waliohudhuria tamasha hilo hali iliyosababisha Waziri Nape kushindwa kuhutubia na kulazimika kuketi chini na Mbunge wa Nyamagana, Stanslaus Mabula alisimama kujaribu kuokoa jahazi, lakini naye akakumbana na kimbunga cha sauti za wananchi walioamua kulitaja jina la mbunge wa zamani wa jimbo hilo, Ezekia Wenje.
Akizungumzia tukio hilo, Nape alisema wananchi waliompigia kelele za “Bunge Live” walisukumwa na masuala ya kisiasa, ndiyo maana aliepuka kuendelea kuzungumza ili kutochafua hali ya hewa uwanjani.
“Pale uwanjani tulikwenda kwa ajili ya burudani, sasa baada ya kuona wananchi wanaanza kuleta masuala ya kisiasa nikaona ni busara kuacha kuhutubia. kuepusha shari,” alisema Nape.
Nape alitangaza uamuzi wa kusitisha kurusha moja kwa moja baadhi ya shughuli za Bunge, akisema Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) linashindwa kumudu gharama, lakini wabunge, hasa kutoka vyama vya upinzani wamepinga hatua hiyo wakisema inawanyima wananchi haki yao ya kikatiba ya kupata habari kuhusu chombo chao cha kutunga sheria.

clouds stream