Tuesday 18 October 2016

Mbunge CCM ‘Alamba’ Mishahara Hewa Mitano

Tarehe October 18, 2016
mshahara-hewaV 2

Sakata la watumishi hewa sasa limefikia pabaya baada ya msako wa watu wanaolipwa fedha bila kuwapo kazini kumkumba Mbunge Makete (CCM), Profesa Norman Sigalla ambaye alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Songea.

Wadau walishawahi kueleza kuwa msako wa watumishi hewa uliwahusu wafanyakazi wa kaliba ya chini na hivyo kuokoa fedha kidogo, lakini sakata la Profesa Sigalla limeonyesha kuwa hata vigogo serikalini wanahusika.

Profesa Sigalla anadaiwa kupokea mshahara wa ukuu wa wilaya kwa miezi mitano baada ya kuacha kazi hiyo wakati wa Uchaguzi Mkuu na baadaye kuchaguliwa kuwa Mbunge kwa tiketi ya CCM.

Hali hiyo imeisababishia Serikali hasara ya Shilingi milioni 23.

Baada ya kuacha kazi hiyo ya kuteuliwa na Rais, inadaiwa kuwa Profesa Sigalla aliendelea kupokea mshahara wake wa Ukuu wa Wilaya wa Shilingi milioni 4.6 kutokana na ofisa utumishi wa ofisi ya katibu tawala wa Mkoa wa Ruvuma kumrudisha kwenye orodha ya malipo ya mshahara.

Katibu Tawala (RAS) Mkoa wa Ruvuma, Hassan Bendeyeko alisema baada ya kufutwa kwenye orodha ya mishahara ya watumishi wa serikali kutokana na kuteuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuwa mgombea ubunge wa Jimbo la Makete,Profesa Sigalla aliendelea kuchukua mshahara hadi mifumo ya uthibiti ilipombaini kuwa analipwa mishahara miwili, wa ubunge na Serikali.

clouds stream