Thursday 23 June 2016

Rais Kagame Kutua Nchini Julai 1


Tarehe June 23, 2016
Rais wa Rwanda, Paul Kagame.
Rais wa Rwanda, Paul Kagame anatarajiwa kufanya ziara rasmi ya kitaifa nchini Julai 1, mwaka huu ambapo pamoja na mambo mengine, atafungua Maonesho ya 40 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (DITF) maarufu  kama Sabasaba kutokana na mwaliko rasmi wa Rais, Dkt. John Magufuli.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi, Dkt. Augustine Mahiga amesema ziara hiyo ni mwendelezo wa uhusiano mzuri baina ya nchi hizo mbili.
Amesema Rais Magufuli amemualika Rais Kagame kuja nchini kutokana na ziara yake aliyoifanya nchini Rwanda mapema Aprili mwaka huu ambayo pamoja na mambo mengine, marais hao walikubaliana kushirikiana kwenye nyanja mbalimbali.
“Rais Magufuli amenituma kuwaambia umma kwamba amemwalika Rais Kagame kuja nchini kwa ziara ya kitaifa ambapo atafungua Maonesho ya Sabasaba na pia watasaini mkataba wa makubaliano kwenye mambo waliyoafikiana wakiwa Rwanda,” amesema Balozi Mahiga.
Katika ziara ya Rais Magufuli nchini Rwanda ambako yeye na Rais Kagame walifungua Daraja la Rusumo lililo mpakani mwa nchi hizo, viongozi hao waliafikiana kuendeleza ushirikiano katika sekta tofauti ikiwemo biashara.
Hata hivyo, marais hao waliwataka wataalamu wa nchi hizo mbili kukaa pamoja na kujadiliana kwa kina mambo waliyozungumza ya ushirikiano, na ujio wa Rais Kagame nchini una lengo pia la kuweka saini ya makubaliano baina yake na Rais Magufuli kwenye Mkataba wa Makubaliano wa ushirikiano wa mambo waliyoafikiana.
Aidha, Balozi Mahiga amesema baada ya Rais Kagame kusaini mkataba huo na mwenyeji wake na kufungua maonesho hayo, jioni ataungana na Rais Magufuli kwenye dhifa itakayoandaliwa Ikulu.
Ziara yake nchini Rwanda ilikuwa ya kwanza nje ya nchi kwa Rais Magufuli tangu achaguliwe kuiongoza Tanzania na kuapishwa Novemba 5, mwaka jana.

clouds stream