Thursday 2 June 2016

Wapinzani Wawasilisha Hoja Ya Kumuondoa Madarakani Naibu Spika


Wabunge wa upinzani wamewasilisha kwa Spika wa Bunge hoja ya kumwondoa madarakani Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kwa kutokuwa na imani naye.

Hatua hiyo imefikiwa na wabunge hao kufuatia kutoridhishwa na mwenendo wa uongozi wa Dk Tulia anapokalia kiti cha Spika. Uamuzi huo ulifikiwa baada ya Dk Tulia kuzuia kujadiliwa hoja ya kufukuzwa kwa wanafunzi zaidi ya 7,000 wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) iliyowasilishwa na Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari.

Kitendo hicho kiliwafanya wabunge wote wa upinzani kupingana na maamuzi ya Dk Tulia, jambo lililosababisha watolewe bungeni.

Kutokana na hali hiyo wabunge hao kupitia Mbunge wa Simanjiro, James Ole Millya akisindikizwa na Mbunge wa Kibamba, John Myika wa Chadema na Mbunge wa Konde wa CUF, Khatibu Said Haji waliwasilisha hoja hiyo kwa Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashilillah baada ya Spika, Job Ndugai kutokuwapo bungeni.

 Kwa mujibu wa Ibara ya 85(4)(c), Naibu Spika atakoma kuwa Naibu Spika na ataacha kiti cha Naibu Spika endapo ataondolewa kwenye madaraka ya Naibu Spika kwa azimio la Bunge.

clouds stream